Jumatano, 31 Agosti 2016

Sheria dhaifu zinawapa kiburi madereva wa bodaboda



Na Shadrack Sagati
Afisa Mfawidhi wa Sumatra Mkoa wa Iringa, Patel Ngereza
 amesema sheria  zinazotumika mahakamani kuwahukumu wakosaji wa makosa ya barabarani ni dhaifu.

Akizungumza na gazeti hili, Ngereza alisema madereva wengi wamezoea kulipa faini na wanaona kama ni jambo la kawaida.

“Ipo haja kwa mahakama kuwatoza faini na kuwafunga kwa makosa yanayofikishwa mahakamani, hii itawaogopesha na kuwafanya wazingatie sheria,” anasema.

Kuhusu sheria hizo, Kamanda wa Kikosi cha Usalama Barabarani anasema mapendekezo yao faini ianzie Sh 100,000 na kifungo kiwe cha zaidi ya mwaka mmoja.

“Kati ya Machi na April mwaka huu makamanda wa usalama barabarani tulikutana Morogoro na tukaja na mapendekezo hayo mapya ya adhabu za makosa ya barabarani, tunaomba wabunge watusaidie kuyapitisha pale yatakapofikishwa bungeni” anasema.

Anasema takwimu za kimataifa zinaonesha asilimia 51 ya ajali zote duniani zinasababishwa na pikipiki kwahiyo kama nchi inataka iwe huru na ajali ni lazima sheria za adhabu za makosa ya barabarani ziwe zinafanyiwa mabadiliko ya mara kwa mara.


Mwenyekiti wa Chama cha Bodaboda (CBBI) mkoani Iringa Hassan Abdul akizungumzia adhabu za hizo, alisema  ukubwa wa adhabu hizo unashawishi rushwa na zinawafanya baadhi ya madereva wasibadilike.

“Rushwa imewafanya baadhi ya madereva hao wawe watukutu, waendelee kutozingatia sheria za usalama barabarani. Pamoja na kutozingatia sheria hizo utukutu wa madereva hao umevuka mipaka hadi kwa abiria wao,” anasema.


Naye Mwenyekiti wa UBBM Makarius Changula ambaye anakiri kuwahi kukamatwa kwa kuendesha pikipiki isiyo na bima anasema adhabu kwa madereva wa bodaboda ziangaliwe upya kwani ni kubwa.

“Adhabu ni kubwa sana, zinachochea rushwa na nikiri baadhi ya askari wa pikipiki, wanapokea sana rushwa kwasababu wanajua hatuwezi kulipa faini kubwa wanazotutoza, hiyo maana yake ni kwamba tutaendelea kufanya makosa ya barabarani na kwa kuzingatia madereva wapya wa bodaboda wanazaliwa kila siku na kuingia barabarani bila kujali sheria zilizopo,” alisema.

Anasema mfumo wa utekelezaji wa sheria za usalama barabarani na zile za Sumatra ni wa kikandamizi kwasababu umeshindwa kuzitofautisha bodaboda ambacho ni chombo cha chini kabisa cha moto na vingine vikubwa zaidi yake.

Changulla anapendekeza faini kwa kosa la barabarani au lolote linalohusiana na biashara yao iwe Sh 10,000 kwa kosa moja.

Akizungumzia pikipiki zinazokamatwa kwa makosa yanayohusiana na ukosefu wa stika za Bima, Changulla anasema gharama yake ni Sh 65,000 kwa mwaka, lakini pamoja na wamiliki wengi wa bodaboda hizo kulipa kiasi hicho kila mwaka, hakuna rekodi inayoonesha kuna msaada wanaopata kutoka katika makampuni ya Bima pindi wanapopata ajali.

“Pikipiki yako iharibike, dereva au abiria wako uvunjike au kupata madhara mengine yoyote yale, hakuna fidia yoyote. Sasa kwanini tuendelee kulipia stika za Bima, malipo hayo ni kwa ajili ya kumnufaisha nani kama hawana msaada wowote,” anasema.

Anasema katika ofisi ya chama chake, kuna madereva wanachama wa UBBM zaidi ya 120 waliopata ajali katika mazingira tofauti lakini hakuna hata mmoja aliyepata fidia toka katika hayo makampuni ya Bima.

ends

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni